WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, kupitia timu ya wataalamu kutoka Ofisi yake, amefanikisha kupatikana kwa suluhu ya mgogoro wa fidia ya ardhi kati ya Kampuni ya Tanganyika Leisure Limited ya Moshi mkoani Kilimanjaro na Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, ambapo kampuni hiyo imekubaliwa kulipwa fidia ya awali ya shilingi milioni 80 kwa eneo lililotwaliwa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Bahari (DMI) katika eneo la Kimbiji, Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya vikao vya maridhiano vilivyodumu kwa siku tano na kuwahusisha wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, wataalamu wa ardhi pamoja na mwakilishi wa kampuni hiyo.
Februari 26, 2026, Mkurugenzi wa Kampuni ya Tanganyika Leisure Limited, Bi. Evetha Massawe, alimwandikia barua Waziri Mkuu akiomba Serikali imsaidie kupata fidia ya eneo la kampuni yake lililotwaliwa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Bahari, akieleza kuwa malipo ya fidia yalikuwa yamechelewa kwa muda mrefu.
Bi. Massawe alidai kuwa tangu mwaka 2022 kampuni yake ilishindwa kuendelea na uwekezaji uliokuwa umepangwa baada ya kupewa taarifa kuwa eneo hilo limetwaliwa kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa Chuo cha Bahari na kwamba fidia ingetolewa.
Kufuatia malalamiko hayo, hivi karibuni Waziri Mkuu alituma timu ya wataalamu kutoka Ofisi yake kwenda kushughulikia mgogoro huo kwa njia ya maridhiano, hatua iliyopokelewa kwa ushirikiano na pande zote zilizohusika.
Katika vikao hivyo vya maridhiano vilivyowahusisha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, Bw. Erasto Kiwale, wataalamu wa ardhi akiwemo Bw. Daimoni Mpoki na Bw. Alphonce Chuwa pamoja na Bi. Massawe, ilikubaliwa kuwa Kampuni ya Tanganyika Leisure Limited ilipwe fidia ya awali ya shilingi milioni 80 huku malipo mengine yakifanyika baada ya kukamilika kwa tathmini mpya ya eneo husika.
Ujenzi wa Chuo kipya cha Bahari katika eneo la Kimbiji lenye ukubwa wa ekari 13 unatarajiwa kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa kuongeza miundombinu ya kisasa ikiwemo madarasa, mabweni na vifaa vya mafunzo vitakavyoongeza uwezo wa chuo hicho kuhudumia wanafunzi wengi zaidi.
Aidha, kuhamishwa kwa shughuli za Chuo kutoka eneo lake la sasa kutatoa fursa kwa Bandari ya Dar es Salaam kutumia eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu itakayoongeza ufanisi wa shughuli za bandari na kuchochea ukuaji wa uchumi.