Mahakama ya Seoul imemhukumu Rais wa zamani wa Korea Kusini, Yoon Suk-yeol, kifungo cha miaka 30 gerezani kufuatia kuhusika kwake katika operesheni ya Ndege zisizo na rubani (droni) zilizodaiwa kurushwa kuelekea Korea Kaskazini.
Kwa mujibu wa Waendesha Mashtaka, operesheni hiyo ililenga kuchochea hali ya taharuki na kuandaa mazingira ya kutangaza Sheria ya Kijeshi mwaka 2024, jambo lililosababisha mvutano mkali wa kisiasa na Kijeshi kati ya Korea Kaskazini na Korea Kusini.
Aidha, droni hizo zimeripotiwa kutawanya vijikaratasi vya propaganda ndani ya eneo la Korea Kaskazini, hatua iliyochochea ongezeko la taharuki katika mpaka wa Nchi hizo mbili ambazo bado zipo katika hali ya uhasama wa muda mrefu.
Mahakama hiyo imesema ushahidi uliowasilishwa ulionesha kuwa hatua hizo zilihatarisha usalama wa Taifa na kudhoofisha utulivu wa kikanda, licha ya Yoon Suk-yeol kukana kuhusika na kutoa amri hiyo.
Hata hivyo, hukumu hiyo imeongeza mfululizo wa maamuzi mazito dhidi ya Kiongozi huyo wa zamani, ambaye tayari alikuwa ameondolewa madarakani kupitia mchakato wa kikatiba ulioidhinishwa na Mahakama ya Kikatiba ya Nchi hiyo.
#MillardAyoUPDATES