Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma limemkamata Filbert Philimon (23), Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha St. John’s kwa tuhuma za kuhusika katika tukio la kuchoma moto chumba kilichosababisha vifo vya Wanafunzi wawili, Rebeka James na Felister Peter.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, leo 14 Juni 2026 ni kwamba tukio hilo lilitokea Juni, 7 2026 majira ya saa mbili usiku katika Mtaa wa Kikuyu, Jijini Dodoma.
Polisi wamesema baada ya kufanya uchunguzi wa haraka na kutumia mbinu za kiintelijensia, walibaini uwepo wa ushahidi uliomuhusisha Mtuhumiwa huyo na hatimaye kumkamata Juni 13, 2026 Magufuli Bus Terminal akiwa katika harakati za kutoroka mkono wa Sheria.
Inadaiwa Mtuhumiwa amekiri kuhusika na tukio hilo na kueleza kuwa alitumia lita mbili za petroli katika kutekeleza uhalifu huo. Chanzo kinachodaiwa ni mgogoro wa kimapenzi baada ya uhusiano wake na marehemu Felister Peter Francis kuvunjika na kuingia kwa Mwanaume mwingine.
Jeshi la Polisi limetoa wito kwa Vijana hususan Wanavyuo kujiepusha na vitendo vya kihalifu vinavyotokana na hasira, wivu na msongo wa mawazo, na badala yake kutafuta ushauri wa kitaalamu ili kukabiliana na changamoto za kisaikolojia na mahusiano kwa njia sahihi.
#MillardAyoUPDATES