TANZANIA HAIKUWA KOLONI; UHURU NI WA TANGANYIKA
Anaandika Baba Askofu Rev.Dr.Benson Bagonza (PhD), Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Karagwe.
-------
Miaka 64 imepita tangu Tanganyika ipate uhuru kutoka kwa “Mdhamini” wetu Uingereza. Mkoloni wetu wa kweli alikuwa Mjerumani. Kiuhalisia Mdhamini na Mkoloni walikuwa ni wale wale tu. Leo 9/12/2025, tumeisherehekea siku ya uhuru tukiwa uani, bandani, mnyororoni na ndani. Tofauti yetu na walio Keko, Ukonga na Segerea ni ndogo: Wanakula kwa kengere, tunakula tukisikia njaa. Tutafakari:
1. Tanzania ilizaliwa 1964 kwa hiyo haikutawaliwa na mkoloni toka Ulaya. Leo tunakumbuka uhuru wa Tanganyika isiyokuwepo lakini ardhi na watu wake vipo. Kama Zanzibar wamepumzika leo, ni kwa ajili ya ujirani mwema. Siku hii kihistoria haiwahusu.
2. Watu wengi hawana shida na Tanzania. Wana shida na Tanganyika. Tanzania ni tunda la Tanganyika. Kama Tanzania ina shida, itafute kaburi la Tanganyika. Mbona tunaendaga kwenye kaburi la Baba wa Taifa?
3. Uhuru hauna hesabu: Kilo, mita, kimo, kina wala nyuzi joto. Uhuru ni utu, heshima, thamani na tunu yetu. Viongozi na watawala wetu wana ruhusa ya KUULINDA na KUUONGEZA tu.
4. Tofauti za mitazano kuhusu uhuru ndio utajiri wetu. Waasisi wetu walilenga tupate uhuru wa kujieleza, kukusanyika, kuabudu, na kujitawala. Barabara, shule, reli, ndege na Mwendokasi ni matunda ya Uhuru SI uhuru wenyewe. Tusirogwe kulinganisha vitu na uhuru wetu.
5. Kama tusivyotaka mataifa mengine kutuamulia mambo yetu, ndivyo tusivyopenda watumishi wetu (viongozi) kuupunguza uhuru wetu kwa kisingizio chochote. Hatukuwakataa wakoloni kwa sababu ya rangi zao. Tulikataa matendo yao yaliyokuwa yanatunyima uhuru na kutufanya tukae bandani kama kuku!
6. Waasisi wa Taifa hili waliutafuta uhuru wetu bila kumwaga damu. Waliudai bila woga. Kuogopwa ni sifa na hulka ya mkoloni. Viongozi wetu waikatae sifa hii. Taifa huru ni watu huru. Tulipokataa ukoloni, tulikataa na hofu (fear) iliyoletwa na ukoloni. Hatuwezi kurejesha hofu bila kurejesha ukoloni. Uhuru na hofu ni maadui wa milele.
7. Maridhiano yanahitaji uhuru. Bila uhuru maridhiano yanatawaliwa na NDIYO kutoka upande mmoja na HAPANA upande wa pili. Mazingira haya yamezalisha kizazi cha serikali yenye ujuzi mdogo katika kukabili hoja na migogoro (critical engagement and dialogue). Tamaa ya “Ushindi” na kilevi la madaraka ni sumu ya maridhiano.
8. Kuadhimisha tukiwa tumefungiwa majumbani huku mitaa imejaa maaskari kama tuko vitani ni ushahidi wa kushindwa kukabiliana kwa hoja na makundi haya:
- Wapinzani
- Jumuia ya kimataifa
- Wapinzani ndani ya vyama vya siasa
hasa ndani ya chama tawala
- Kizazi kipya ( Gen - Z)
- Jumuia za kiimani
- Asasi za kiraia
- Majirani zetu nk
Ukiangalia kiwango cha uvujishaji wa siri, kimya cha waliotazamia kusema, sauti za waliokuwa kimya na mwangwi wa kutengwa kwetu kama taifa, unaona ombwe kubwa katika weredi wa kukabili kwa hoja. Mtutu haujadili. Ukichoka kutazama mbele, unatazama nyuma. Shtuka.
9. Tabia moja ya utawala usiokuwa tayari kukabiliana (Engage) na maridhiano, ni kuchelewa kufanya maamuzi au kutegeana katika kufanya maamuzi. Matokeo yake ni kutumia suluhisho la juzi kwa tatizo la leo. Msingi wa maridhiano yoyote ni kuweka silaha chini, minyororo yote chini, malango ya magereza yawe wazi, madaraka yote yawe chini isipokuwa mamlaka.
10. Wajaluo wanafundisha kuwa “si kila Uhalali wa kisheria unaendana na kukubalika” (Legality versus Legitimacy). Tumefanya uchaguzi kisheria lakini kukubalika kwake kunahojiwa hata na waliousimamia. Uchaguzi ulikosa uaminifu na uangalifu. Serikali siyo malaika na malaika siyo serikali. Serikali, bunge na mahakama ni mali ya wananchi. Wasikilizeni. Msisikilize washauri maana wako kwenye ajira. Mkichelewa, siku isiyo leo, Mjaluo atajifunza kiingereza.
“ Kristo alituweka sisi huru ili tuwe huru.
Kwa hiyo simameni imara, wala msikubali tena kulemewa na minyororo ya utumwa”.
WAGALATIA 5:1