Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amesema serikali haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya watu watakaojaribu kuvuruga amani na utulivu katika mkoa huo na nchini kwa ujumla.
Akizungumza leo June 15, 2026 katika kikao kilichowakutanisha wenyeviti wa mitaa na watendaji wa kata kilichofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), Chalamila amesema amekuwa akifuatilia baadhi ya mijadala inayofanyika mitandaoni na kubaini kuwa kuna watu wanaotamani kuleta chokochoko katika maeneo mbalimbali.
"Nimeona pia kwenye mitandao baadhi ya watu wanatamani kuleta chokochoko kwenye mikoa yetu, na kwa bahati mbaya sana nguvu inayotumika katika kulinda amani wakati mwingine inakuwa ya kawaida sana," amesema Chalamila.
Mkuu huyo wa Mkoa aliongeza kuwa mamlaka za serikali zitaendelea kuhakikisha amani na usalama vinadumishwa, akionya kuwa hatua kali zaidi zinaweza kuchukuliwa dhidi ya yeyote atakayehatarisha utulivu wa nchi.
"Nimeona pia kwenye kikao hiki nije niwaeleze kwamba, nguvu zitakazoendelea kutumika kulinda amani pengine haijawahi kutokea wala kuonwa katika kipindi chote, na pengine kuna wengine wanadhani kuna nguvu ishawahi kutumika mahali. Kwenye kikao hiki nataka niwathibitishie yalikuwa ni majaribio kutumia nguvu kulinda amani," amesema.
Kauli hiyo imekuja wakati kukiwa na mjadala unaoendelea kuhusu hali ya kisiasa nchini, huku viongozi wa serikali wakisisitiza umuhimu wa kulinda amani, usalama na utulivu wa taifa.
Kikao hicho kilihusisha viongozi wa ngazi za mitaa na kata, ambao walijadili masuala mbalimbali yanayohusu utawala wa maeneo yao, ushirikishwaji wa wananchi na uhifadhi wa amani katika jamii.